Jumamosi, 25 Juni 2016

SERIKALI YASITISHA KAULI YAKE YA CHAKULA HOSPITAL YA MUHIMBILI


Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya jamii, Jinsia, Wazee na Watoto , imesitisha tamko la utoaji wa vyakula kwa wagonjwa watakaolazwa katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili ili kupisha utafiti wa kina kuhusu huduma hiyo ili kuweza kutoa kilicho bora kwa watanzania.


Akizungumza hayo leo jijini Dar es salaam Waziri wa Afya, Maendeleo ya jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bi. Ummy Mwalimu amesema kwamba wameamua kusitisha mpango mpaka watapotangaza tena ili kufanya utafiti kujua kama kuna faida au hasara kwa wananchi.


“Natoa tamko kwamba huduma hii iliyotarajiwa kuanza hivi karibuni isitishwe mara moja ili kupisha watafiti waweze kufanya uchunguzi kujua inawasaidia kwa kiasi gani wananchi”alisisitiza Bi. Mwalimu.


Aidha Bi. Mwalimu amesema kwamba huduma hiyo itatolewa kwa wagonjwa watakaolazwa hapo kwa kulipia shilingi elfu 50 ikiwemo shilingi elfu kumi ya kumuona daktari , elfu kumi ya kitanda na elfu 30 iliyobaki ni kwa malipo ya chakula kwa wiki.


“Huduma hii inalenga kuwasaidia wananchi katika kuwaandalia chakula stahiki kwa wagonjwa na kupunguza usumbufu kwa waangalizi wa wagonjwa wao kuleta vyakula hospitalini ili kuimalisha afya zao kwa ujumla”aliongeza Bi.Mwalimu.

Alhamisi, 16 Juni 2016

POLISI YAVAMIA NYUMBA YA GWAJIMA


Taarifa zilizotufikia muda huu zinasema Polisi 6 wakiwa ndani ya Landcruiser wamezingira nyumbani kwa Askofu Josephat Gwajima. 


Sababu za kufanya hivyo bado hazijafahamika, tutaendelea kuwajuza kadri tunavyoendelea kupata taarifa.

WATANZANIA ASILIMIA 100 WANATAKA BUNGE LIONESHWE LIVE


TAASISI ya Twaweza imetoa matokeo ya utafiti wake, ambapo imebainika kuwa asilimia 79 ya Watanzania wamepinga uamuzi wa Serikali wa kusitisha matangazo ya moja kwa moja (Live ) ya Bunge.


Katika maoni yao, wananchi hao wamedai kuwa ni haki yao ya msingi kufahamu kinachoendelea katika vikao mbalimbali vya Bunge.


Utafiti wa taasisi hiyo umefanywa katika maeneo tofauti ya Tanzania Bara kupitia mpango wake wa Sauti za Wananchi.


Akitoa taarifa ya matokeo ya utafiti huo jana jijini Dar e Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa Twaweza, Aidan Eyakuze,  alisema suala hilo limeonekana kutokuungwa mkono na wananchi wengi.


“Asilimia kubwa ya Watanzania wanapinga uamuzi wa Serikali wa kusitisha matangazo ya moja kwa moja ya Bunge. Suala hili limeonekana kugusa hisia za watu wengi na maamuzi haya ya Serikali yakionekana kutoungwa mkono.


“Katika utafiti huu wananchi nane kati ya 10 wanapinga uamuzi wa hali inayodhihirisha kutoungwa mkono kwa hatua hiyo,” alisema Eiyakuze.


Akizungumzia sababu walizozitoa  wananchi wanaotaka matangazo ya Bunge yarushwe moja kwa moja,  Eiyakuze alisema asilimia 46 walisema yanawafanya waweze kufuatilia utendaji wa wabunge waliowachagua kwa kuwa huko ndio walikowatuma.


“Asilimia 44 wanasema ni muhimu kwa sababu wananchi wanahaki ya kufahamu kinachoendelea bungeni, asilimia 29 wanasema matangazo ya moja kwa moja yalikuwa yanaaminika zaidi kwa watazamaji na wasikilizaji  kuona na kusikia wenyewe kile kinachoendelea tofauti na mfumo wa kurekodi ambapo kuna baadhi ya mambo yanahaririwa.


“Asilimia 16 walidai kuwa inafursa mwananchi kupata taarifa sahihi badala ya kuzisoma kwenye magazeti huku asilimia 16 nyingine wakisema inawasaidia wanachi kufuatilia mijadala ya Bunge kwa wakati”, alisema Eiyakuze.


Pamoja na hali hiyo mkurugenzi huyo alisema katika utafiti huo asilimia 92  ya wananchi walisema kuna umuhimu wa vipindi vya Bunge kurushwa moja kwa moja kupitia Luninga na redio bila kujali gharama zilizoelezwa kuwa ndio chanzo cha kufikia uamuzi huo.


“Asilimia 88 walisema vipindi vya Bunge virushwe ‘Live’ bila kujali gharama ukilinganisha na asilimia 12 ambao waliona ni muhimu suala la bajeti likazingatiwa,” alisema.


Mkurugenzi huyo alisema asilimia 80 wanaona matangazo ya moja kwa moja kutoka bungeni ni muhimu kama yalivyo na asilimia 20 wakisema fedha hizo zitumike kwenye huduma nyinge za jamii.


Akizungumzia suala la vyombo vya habari vya binafsi kuruhusiwa kurusha matangazo hayo,  Eiyakuze alisema wananchi wanaunga mkono vyombo hivyo kuruhusiwa iwapo Serikali imeshindwa kumudu gharama.


Utafiti huo pia umeonesha Watanzinia wanne kati ya kumi wamewahi kuangalia matangazo ya moja kwa moja kupitia Luninga na sita kati ya kumi  wamesikiliza kupitia redio.


Aidha utafiti huo umeonyesha zaidi ya nusu ya wananchi walosema wameangalia au kusikiliza vipindi vya Bunge wamefanya hivyo ndani ya miezi miwili iliyopita.


Hali ilivyokuwa

Januari mwaka huu, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo,  Nape Nnauye, alitoa ufafanuzi bungeni kuhusu hatua ya Serikali kusitisha matangazo hayo kupitia Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC).


Miongoni mwa sababu alizozieleza ni pamoja na kuwepo kwa gharama kubwa ya Sh bilioni 4.2 zinazotumika katika uendeshaji wa matangazo hayo ya moja kwa moja kwa mwaka pia watumishi wa serikali kushabikia Bunge badala ya kuendelea na kazi ofisini.


Hatua ya Serikali kusitisha matangazo hayo iliibua mjadala mkubwa bungeni huku Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe, (ACT-Wazalendo) akilitaka Bunge kusitisha shughuli zake ili kujadili taarifa hiyo ya Serikali.


Siku chache baadaye kilio hicho cha ukosefu wa fedha za kuonesha matangazo hayo ya moja kwa moja ambacho kimekuwa kikitolewa na serikali, sasa kilipata ufumbuzi.


Hatua hiyo iliyokana na uamuzi wa Mfuko wa Vyombo vya Habari nchini (TMF), kujitokeza hadharani na kueleza kwamba upo tayari kutoa fedha zinazohitajika ili kuhakikisha haki ya Mtanzania kupata habari kupitia TBC haiingiliwi wala kubughudhiwa kwa hoja yoyote.


Endapo Serikali itakubali ombi hilo, wananchi wataendelea kunufaika na vikao vya moja kwa moja vya Bunge tofauti na pendekezo la serikali la kunakili baadhi ya sehemu na kisha kuoneshwa usiku.

Jumatano, 15 Juni 2016

SIMU FEKI KUZIMWA RASMI KESHO




SIMU ziliingizwa nchini zikiwa hazina kiwango kuzimwa rasmi kesho, katika kuhakikisha kila mtu anatumia simu kiwango kwa usalama  na ulinzi wa nchi.


Akizungumza na waandishi habari jijini Dar es Salaam, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano nchini (TCRA), Mhandisi James Kilaba amesema kuwa katika uzimaji wa simu wameshatoa elimu juu ya simu hizo.


Kilaba amesema kuwa simu ambazo watu walibadilisha (Flash) nazo zitazimwa kutokana na kufanya hivyo ni kosa la kisheria na mtu anayefanya hivyo kifungo chake ni miaka 10.


Amesema hakuna kitu chochote kinachofanya simu zisiweze kuzimwa hivyo watu wajiandae kwa zoezi hilo na simu zitakazozimwa wametakiwa kuzihifadhi katika mazingira salama.


Aidha amesema wametoa elimu ya kutosha, hivyo kesho kutakuwa na mkutano wa wadau mbalimbali wa makampuni ya simu, na wamiliki wa maduka ya simu pamoja na mafundi katika kubadilishana mawazo wakati wa kuzima simu feki.


‘’Simu feki kesho zitazimwa, hatutakuwa na mabadiliko ya kuongeza muda au vinginevyo kutokana na elimu iliyotolewa juu ya simu ya  feki ambazo baada ya soko kushindikana mjini walipeleka vijijini’’amesema Kilaba  .

Jumanne, 14 Juni 2016

Lipumba wamkataa cuf


Wakati aliyekuwa Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba akitengua uamuzi wake wa kung’atuka kwenye wadhifa huo na kuomba kurejea, viongozi wa juu wa chama hicho wamepinga hatua hiyo wakisema katiba yao hairuhusu na kwamba anakwenda kukiua chama.


Kauli za viongozi hao, zimekuja muda mfupi baada ya Profesa Lipumba kutangaza nia hiyo jana kwenye ofisi za makao makuu ya chama hicho, Buguruni huku akibainisha kuwa amefanya hivyo baada ya kuombwa.


Naibu Katibu Mkuu wa CUF Zanzibar, Nassor Ahmed Mazrui alisema Lipumba hawezi kuwa na nia njema ya kukijenga chama hicho endapo atarudishwa kwenye nafasi aliyoikataa.


“Anataka kuja kukiharibu chama,” alisema Mazrui. Alifafanua kuwa tayari chama hicho kimefanya mambo mengi bila Lipumba ambaye alikuwa anaona kila kinachoendelea, hivyo alichokisema hakina mashiko kwani CUF ilisharidhia kuitisha mkutano wa uchaguzi kujaza hiyo.


Akieleza sababu alizozitoa mwenyekiti huyo, Mazrui alisema haoni chochote cha maana. “Sababu zilizomuondoa zingalipo. Kinachomrudisha ni nini?”alihoji naibu katibu mkuu huyo.


 Alisisitiza kuwa Wazanzibari wanaendelea na mchakato wa kuidai haki yao iliyoporwa Oktoba 25 na hawana nafasi ya kushughulika na masuala yasiyokuwa na tija kwao, hivyo haoni kama kuna sababu ya kumjadili Lipumba na nafasi yake badala ya kuendelea pale walipo.


 “CCM wanaona kinachoendelea, hivyo wameona wamtumie Lipumba kuja kuharibu mipango yetu. Hatuna muda wa kumjadili.Tunataka haki iliyoporwa,”alisisitiza. 


Msimamo wa Mazrui haukutofautiana sana na ule wa Kaimu Mwenyekiti wa chama hicho, Twaha Taslima aliyebainisha kuwa amesikia taarifa za kurudi kwa Profesa Lipumba, lakini haoni uwezekano huo. 


“Katiba hairuhusu hilo.Hakuna kifungu kinachotoa nafasi kwa kiongozi aliyejiuzulu kurudi kwenye nafasi yake pindi atakapotaka kufanya hivyo,” alisema Taslima.


Aliielezea Ibara ya 117 (2) iliyotumiwa na Profesa huyo kuandika barua ya kutengua uamuzi wake, kuwa inatoa tafsiri zaidi ya moja hivyo kuwapo haja ya viongozi kukutana na kujadili suala hilo kabla ya kutoa maamuzi.


Kwa kuwa hakuwapo kwenye mkutano huo, Taslima alisema: “Tunahitaji kukutana haraka na kujadili. Tutafanya mkutano wetu na tutavijulisha vyombo vya habari ndani ya wiki hii.”


Taslima alisema kipindi alichoongoza kilikuwa na changamoto nyingi ambazo ni tofauti na sasa, hivyo haoni haja ya mtu mwingine kuja wakati mambo yametulia. Chama hicho kilipanga kufanya uchaguzi wa kuziba nafasi hiyo Agosti mwaka huu.


Baada ya kung’atuka kwa Lipumba, Taslima alichukua mikoba yake na kukivusha chama hicho kwenye kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka jana, pamoja na ule wa Zanzibar ambao uliahirishwa na chama hicho kususia marudio yake Machi 20 mwaka huu.


Hata hivyo, Mkurugenzi wa Mawasiliano wa chama hicho, Abdul Kambaya alisema upo uwezekano wa Lipumba kurudi kwenye nafasi yake kwasababu mpaka sasa haijazibwa.


“Mwenyekiti huchaguliwa au kutenguliwa na halmashauri kuu. Haikupitisha kujizulu. Barua ya kujiuzulu itaenda pamoja na hii ya kutengua uamuzi wa awali,” alisema Kambaya.


Kauli ya Lipumba 

Awali, Profesa Lipumba alisema mara kadhaa amekutana na viongozi wa dini na chama pamoja na wanachama wa CUF na wote walikuwa na ujumbe mmoja tu…’rudi tukijenge chama.’ 


Profesa Lipumba hakushiriki mchakato wa uchaguzi mkuu wa Oktoba 25, mwaka jana ambao kwa upande wa Zanzibar, kutokana na hitilafu zilizojitokeza ulifutwa na kurejewa Machi 20 mwaka huu huku chama hicho kikiwa kimesusia marudio hayo. 


Pamoja na hayo yote, Lipumba alisema ametafakari sana juu ya hali ya kisiasa Zanzibar na kuona umuhimu wa kutoa ushirikiano ili mambo yaende kwa manufaa ya taifa. 


“Ni lazima nchi iendeshwe kwa misingi ya demokrasia ambayo itapatikana kwa umoja wetu.Nimerudi kushirikiana na wenzangu kutimiza malengo hayo ili kuchangia maendeleo ya Tanzania,”alisema Profesa Lipumba. 


Lipumba aliachana na uongozi wa chama hicho, Agosti 8, mwaka jana, siku chache baada ya vyama vinavyounda Ukawa kukubaliana kumsimamisha Edward Lowassa.


Alimuandikia barua Katibu Mkuu wake, Maalim Seif Shariff Hamad kuwa hakubaliani na uamuzi wa chama chake kuridhia makada waliohama Chama cha Mapinduzi (CCM), akiwemo Lowassa, kupewa fursa ya kugombea nafasi za uongozi.


Baada ya kukatwa kwenye mchujo wa ndani ya CCM, Lowassa akiwa na makada kadhaa wa chama hicho akiwamo aliyewahi kuwa waziri mkuu, Frederick Sumaye, alihamia Chadema ambako alipewa fursa ya kupeperusha bendera ya chama hicho kilichomo ndani ya Ukawa.


Lipumba hakukubaliana na hilo, alikaa pembeni na kuachia ngazi ingawa alishiriki tukio la kumkaribisha Lowassa ndani ya Ukawa.


Jana, wakati anatangaza kufanya mabadiliko ya kile alichokiamua miezi 10 iliyopita, hakuruhusu maswali, ila alifafanua kile kitakachofuata baada ya kuwasilisha ombi hilo, kwa mujibu wa Katiba ya chama hicho: “Katibu Mkuu anashauriana na wanasheria kabla suala langu halijapelekwa kwenye halmashauri kuu kama katiba inavyosema,” alisema Profesa Lipumba.

KADA WA CCM CHARLES MWAKIPESILE AWASHANGAA WAPINZANI

Jumatatu, 13 Juni 2016

CHEKA KIDOGO NA VITUKO VYA JOTI

UVCCM MKOA WA MBEYA NA SONGWE WATOA TAMKO LA KUMUUNGA MKONO NAIBU SPIKA DR. TULIA ACKSON


Mwenyekiti wa Uvccm mkoa wa mbeya na songwe Aman kajuna ametoa tamko la Umoja wa vijana (UVCCM) la kumuunga mkono mh. Dr. Tulia Akson Naibu spika wa bunge la jamuhuri ya muungano wa tanzania .Akisoma risala mbele ya waandishi wa habari alisema wanasikitishwa na kulaani vikali na vitendo vinavyofanywa na wabunge wa upinzani vya kutaka kumhujumu naibu spika kwa sababu zao binafsi zisizo na maslahi kwa umma isipokuwa kwa vyama vyao pekee kwani uwezi kumuondoa naibu spika kwa kusimamia kanuni na taratibu zilizotungwa na wao wenyewe waheshimiwa wabunge na kuwanyima wananchi waliowachagua .Rai yao kwa wapinzani Wanawashauri wapinzani kurejea maneno ya busara yaliyotolewa na Dr. Harrison Mwakyembe. UVCCM imewaomba wabunge wa upinzani walejee bungeni kuwawakilisha wananchi waliowachagua kwa kuwatetea kwa hoja za msingi zenye maslahi kwa taifa na sio vyama vyao Pekee.

MASHINDANO YA KIMONDO CUP YAFUNGULIWA RASMI


Mashindano ya Kimondo Cup hatimaye yamezinduliwa siku ya Jana katika uwanja wa mlangali wilayani mbozi Mkoa wa Songwe. Akitoa risala fupi Mh. Diwani wa kata ya mlangali ambaye pia ni Mwenyekiti wa halimashauri ya Mbozi Erick Ambakisye alisema mashindano hayo yamekuwa na changamoto nyingi ikiwemo uendeshaji wake umekuwa mgumu Sana ukizingatia mashindano hayo hayana mdhamini.lakini pia alisema faida ya mashindano hayo yameonekana kwa kipindi kilichopita cha miaka miwili kwa kutoa wachezaji kwenda ligi kuu .akiwemo Geofrey mwashiuya anaikipiga timu ya yanga na Geofrey mlawa anaekipiga mbeya city. Naye mgeni rasmi wa ufunguzi wa kimondo cup mkuu wa wilaya ya mbozi mkoa wa songwe mh.Ahmad alisema kwa upande wa serikali itashirikiana kuwasaidia kujenga mahusiano na makampuni ili waweze kudhamini mashindano hayo.

Pamoja na hayo ulipigwa mchezo wa ufunguzi wa mashindano hayo Kati ya mabingwa watetezi wa msimu uliopita wembe fc waliofanikiwa kushinda mchezo huo kwa magoli 2 kwa 1 dhidi ya haterere fc mashindano haya yanatarajia kuanza kesho katika viwanja mbalimbali wilayani mbozi Kata ya mlangali.

Mabingwa watetezi wa Kimondo Cup Wembe Fc wakiwa katika picha ya pamoja kabla  mchezo kuanza wa ufunguzi.

Jumapili, 12 Juni 2016

CHADEMA, CCM Watofautiana Kuhusu Naibu Spika, Dk Tulia Ackson


Wakati Halmashauri Kuu ya CCM mkoani Mbeya ikiutaka uongozi wa Bunge kuwachukulia hatua kali wabunge wa upinzani wanaosusia vikao vya Bunge, Chadema, Kanda ya Magharibi, imemtaka Naibu Spika, Dk Tulia Ackson kujitafakari upya kama anafaa kuendelea na nafasi hiyo.


Kwa nyakati tofauti, viongozi wa CCM na Chadema walitoa kauli hizo ikiwa ni siku ya 12 tangu wabunge wa upinzani kususia vikao vinavyoendesha na Dk Tulia.


CCM walisema kitendo kinachofanywa na Chadema kinachochea siasa za kibaguzi badala ya kufanya kazi ya kutunga sheria ya kusimamia Serikali kwa maslahi ya wananchi.


Katibu wa Siasa Itikadi na uenezi Mkoa wa Mbeya, Bashuru Madodi aliwaambia waandishi wa habari ofisini kwake kuwa kitendo kinachofanywa ni kinyume cha maadili na mwongozo wa nchi na kumpongeza Dk Tulia kwa msimamo wake wa kuliongoza Bunge bila kujali ubabaishaji wa wabunge wa upinzani.


“Kitendo cha wabunge kutoka nje wakati wa vikao na kupiga soga ni utovu wa nidhamu na kutoheshimu kiti cha spika na hivyo wajiulize bungeni walikwenda kwa maslahi ya wananchi au la? ”alihoji.


Madodi alisema pia halmashauri kuu inalaani vikali matamko yanayotolewa ya wabunge wa upinzani ya kuzunguka nchi nzima kufanya siasa za kuwahadaa wananchi kuwa wameonewa bila kutambua kuwa wao ni chanzo cha uvunjifu wa amani kwa kutozingatia na kufuata kanuni na taratibu za Bunge.


Kadhalika alisema ni vyema Bunge kufanya maamuzi ya kutowalipa posho wabunge watakaokuwa wakishindwa kuhudhuria vikao vyake.


“Uongozi wa Bunge usitetereke kwa vitendo vya ubabaishaji wa vyama vya upinzani na uendelee kuchukua hatua stahiki dhidi ya wabunge wanaoendelea na vitendo vya utovu wa nidhamu badala ya kuwasilisha kero za wananchi waliowachagua,” alisema.


Kaimu Katibu CCM Mkoa wa Mbeya, Lobe Zongo alipongeza jitihada zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais John Magufuli ya kurejesha nidhamu ya utendaji wa kazi serikalini hali itakayosaidia uchumi wa nchi kusonga mbele na kurejesha nidhamu.


 “Haya yote ni matunda ya Rais wa awamu ya tano kwa kweli anastahili pongezi kwa uwajibikaji na utendaji wa kazi kwa watendaji ndani ya chama na serikalini,”alisema.


Katibu wa Chadema Kanda ya Magharibi, General Kaduma alimlaumu Tulia akidai hana uchungu na wananchi kwa kuwa hakuchaguliwa kwa kupigiwa kura kama walivyokuwa manaibu waliomtangulia.


 Kaduma alidai Naibu spika huyo amevunja kanuni za Bunge na kuwadhalilisha wabunge wa upinzani kwa kushiriki kuondoa vipengele muhimu katika hotuba ya waziri kivuli wa mambo ya ndani, Godbles Lema.


Katibu huyo ambaye amechukua nafasi ya aliyekuwa Katibu wa Chadema Kanda hiyo, Christopher Nyamwanji, aliitaka Serikali kuingilia kati uamuzi uliotolewa na Kamati ya Maadili ya Bunge akidai hayakuwa sahihi.


“Mchango wa wabunge waliozuiliwa kuingia bungeni ni mkubwa katika Bunge hili la bajeti ila utakosekana kutokana na uamuzi uliochukuliwa na naibu spika ambao kimsingi unaminya demokrasia nchini,” alidai.


Pia, alikemea kitendo cha Jeshi la Polisi kuzuia mikutano na kutumia silaha za moto kutawanya umma akisema kinasababisha uvunjifu wa amani.


Amelitaka jeshi hilo kuacha kufanya kazi kwa maslahi ya CCM na badala yake wawe walinzi wa amani nchini kwa kufanya kazi bila upendeleo.


Mwenyekiti wa Chadema mkoa wa Tabora, Francis Msuka alisema wajibu wa kufanya mikutano ya siasa nchini ni wa muda wote kabla na baada ya Uchaguzi Mkuu mwaka jana.


Alisema kumekuwa na matukio ya viongozi wa Chadema kunyanyaswa na Jeshi la Polisi huku viongozi wake ngazi ya vijiji wakifanyiwa mizengwe ili wasitimize majukumu yao kikamilifu.

Ijumaa, 10 Juni 2016

CHUO CHA ILEMI POLYTECHNICS NI JIPU CHAFUNGWA


Katibu mtendaji wa baraza la elimu ya ufundi( NACTE) amewasilisha tamko kwa Mkuu wa Mkoa wa Mbeya leo akifunge Chuo cha Mbeya polytechnics kwa kosa la KUDAHILI wanafunzi 270 wasiokuwa na SIFA kati ya wanafunzi 359 wa Chuo hicho .Ni wanafunzi 89 tu ndiyo wana sifa . Wanafunzi hao 270 walidahiliwa kwa ajili ya cheti na diploma ya kilimo wakiwa na ufaulu wa masomo ya sanaa na wengine wakiwa hawana ufaulu wowote
Sababu nyingine ni Chuo kutokuwa na mitaala inliyoidhinishwa na wizara ya kilimo
Kufungwa kwa Chuo hicho kufuatia malalamiko ya wanafunzi kwa Mkuu wa Mkoa wa mbeya mei mwaka huu na Mkuu wa Mkoa kuunda kamati iliyokuwa chini ya mkurugenzi wa NACTE kanda , afisa Elimu wa mkoa na maafisa toka ofisi ya Mkuu mkoa kuiwasilisha taarifa kwa Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa mkoa kuikabidhi kwa Katibu wa NECTA na baada ya kujiridhisha kuwa Chuo hicho nimefanya makosa na kuwasilisha tamko kwa Mkuu wa mkoa na kumuelekeza akifunge Chuo hicho rasmi
Mkuu wa mkoa leo ametoa tamko la kukifunga Chuo hicho na wanafunzi 89 wanahamishiwa Chuo cha Mbalizi polytechinic
Aidha Mkuu wa mkoa ameagiza ada zote zilizolipwa na wanafunzi warejeshewe kwa ajili ya kujiunga na vyuo vingine kwa sifa walizonazo na wakiohamishwa ada yao ipelekwe kwenye Chuo wakuvhohamishiwa wanafunzi hao
Ameagiza jeshi la polisi, mmliki wa Chuo na timu iliyoundwa kuratibu na kutekeleza maagizo hayo kuanzia leo

HALMAHAURI YA MBEYA YAKAMILISHA UTENGENEZAJI MADAWATI WAMKABIDHI MKUU WA MKOA WA MBEYA AYAGAWE KWA SHULE 51


Halmashauri ya Mbeya imekamilisha utengenezaji wa madawati 5,371 ikiwa ni agizo la Rais kuhakikisha wanafunzi wote wanakaa katika madawati
Akisoma taarifa kwa Mkuu wa mkoa wa mbeya mkurugenzi wa halmashauri Mbeya Viijini Upendo Sanga amesema wamekamilisha utengenezaji madawati mapema kabla ya juni 30 kwenda sambamba na agizo la Mkuu wa mkoa halmashauri zote zikamilishe madawati tarehe 20 juni siku kumi kabla ya tarehe ya mwisho ya mheshimiwa Rais
Mkuu wa Mkoa amekabidhi madawati 3,746 kwa shule 51 na yaliyobaki ameagiza yaendelee kukabidhiwa kwa Shule zingine
Amesisitiza halmashauri zote kukamilisha utengenezaji wa madawati ifikapo tarehe 20 Juni

Chama cha mapinduzi mkoa wa mbeya yatoa kauli ya kumuunga mkono naibu spika



Katika kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Mbeya iliyokutana tarehe 04.06.2016, ilitoka na maazimia yafuatayo.
Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Mbeya, Inampongeza Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt Tulia Ackson Mwansasu, kwa jinsi anavyolisimamia na kuliongoza Bunge kwa kufuata na kusimamia misingi ya sheria, taratibu na kanuni za Bunge.

Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Mbeya, inalaani kitendo cha Wabunge wa vyama vya upinzani kuonyesha utovu wa nidhamu kwa Bunge kwa kutoheshimu kiti cha Spika.


Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Mbeya, inalaani kitendo cha wabunge wa vyama vya upinzani kutoka nje wakati wa vikao vya Bunge na kwenda kupiga soga nje, huku wakijua kuwa wametumwa na wananchi kwenda Bungeni kuwawakilisha.

Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Mbeya, inalaani kitendo cha wabunge wa upinzani kuendesha siasa Bungeni, badala ya kufanya kazi ya kutunga sheria na kuisimamia Serikali.


Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Mbeya, inalaani matamko ya wabunge wa vyama vya upinzani, ya kuzunguka nchi nzima kwenda kufanya siasa za kuwahadaa wananchi kuwa wameonewa, wakati wao ndio hawataki kufuata kanuni na taratibu za Bunge.
Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Mbeya, Inaunga mkono hatua ya Uongozi wa Bunge kutowalipa posho wabunge wote watakaokuwa wanatoka Bungeni bila ya kufuata utaratibu.

WATUMISHI HEWA 170 WAPATIKANA MBEYA


Serikali Mkoa wa Mbeya imebaini watumishi hewa 170 kutokana na uhakiki ulifanywana timu ya vyombo vya dola iliyoundwa na Mkuu wa Mkoa mbeya tarehe 20 April mwaka huu na idadi ya watumishi hewa imesababisha hasara ya she 773,882,066

Hayo yamesemwa na Mkuu wa mkoa wa Mbeya alipokutana na waandishi wa habari kutangaza matokeo ya timu aliyounda kuhakiki watumishi hewa

Pamoja na hasara hiyo watumishi hewa 58 kati ya 170 wamekopa mikopo katika benki jumla ya shilingi 481,574,351

Serikali pamoja na kufanya uhakiki iliwataka watuhumiwa kurejesha fedha zote katika akaunti na sh 65,058,542

Mkuu wa mkoa amewaagiza wakurugenzi kwa kushirikiana na vyombo vya dola kuwasaka popote walipo watumishi hewa na kuwachukulia hatua za kisheria

Aidha amewaagiza wakurugenzi, maafisa utumishi na maafisa wa mfumo kuwajibika kwa kuendelea kulipa watumishi hewa

Kuanzia sasa kila afisa utumishi atawajibika kuwaondoa watumishi watoro pale wanapobainika na amewataka wakurugenzi kuwa na mipango endelevu ya kudhibiti watumishi hewa.

Alhamisi, 9 Juni 2016

Mchanganuo Mzima wa Bajeti ya Serikali 2016/ 2017 Iliyosomwa Jana Bungeni..... Kujua nini Kimepanda na Nini Hakijapanda

SERIKALI imewasilisha Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2016/2017 ya Sh trilioni 29.53, ambayo nguvu kubwa imewekwa katika kukusanya mapato kwa kulinda viwanda vya ndani na kubana matumizi ya serikali ili kuelekeza sehemu kubwa ya matumizi katika maeneo ya vipaumbele.

Katika bajeti hiyo, bidhaa za lazima zinazogusa maisha ya wananchi ikiwemo mafuta ya petroli na dizeli pamoja na ushuru wa barabara na maji ya kunywa, havijaguswa huku bidhaa za starehe kama bia, sigara, soda, juisi na nyingine kama nguo za mitumba, huduma za kupanga nyumba na uhamishaji fedha kwa simu, vikipandishwa kodi, huku kiinua mgongo cha wabunge, kufutiwa msamaha wa kodi.

Aidha, makusanyo ya mapato yasiyo ya kodi, ikiwemo mapato ya taasisi za udhibiti kama Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Maji na Mafuta (EWURA), Shirika la Viwango (TBS), Jeshi la Polisi (Trafiki) na mamlaka nyingine za udhibiti, sasa yatapelekwa moja kwa moja katika Mfuko Mkuu wa Serikali ambapo mahitaji yao ya fedha yatatolewa na Wizara ya Fedha na Mipango, badala ya kujigawia kutokana na bakaa ya mapato waliyokusanya.

Aidha, maduka ya kutoa huduma katika majeshi, yamefutiwa kodi rasmi na badala yake, Serikali inajipanga kuongeza posho kwa askari, ili iwasaidie kukidhi mahitaji yao, huku taasisi za umma na ofisi zote za Serikali, zikipigwa marufuku kufanya biashara na mzabuni asiyetumia mashine za kodi za kielektroniki (EFD’s).

Kodi juu 
Katika bidhaa zilizoongezewa ushuru na kodi ni pamoja na vinywaji baridi, kutoka Sh 55 kwa lita mpaka Sh 58, huku ushuru wa forodha katika maji ya matunda (juisi) yanayotumia matunda yanayozalishwa hapa nchini, ukipanda kidogo kutoka Sh 10 mpaka 11 kwa lita. Juisi zinazotokana na matunda ambayo hayazalishwi hapa nchini, ushuru wake pia umepanda kutoka Sh 200 kwa lita hadi Sh 210 kwa lita.

Bia, vilevi, mvinyo 
Kwa upande wa bia, serikali imependekeza bia inayotokana na nafaka ya hapa nchini, ambayo haijaoteshwa kama kibuku, ushuru upande kutoka Sh 409 kwa lita mpaka 430.
Bia zingine, ushuru wake pia umepanda ambao sasa utatoka Sh 694 mpaka 729 kwa lita, huku bia zisizo na kilevi, ikiwa ni pamoja na vinywaji vya kuongeza nguvu, ushuru ukipanda kutoka Sh 508 kwa lita mpaka Sh 534.

Kwa upande wa mvinyo uliotengenezwa kwa zabibu zilizolimwa nchini kwa kiwango cha asilimia 75, ushuru wake umepanda kutoka Sh 192 kwa lita mpaka Sh 202. 
Ushuru wa mvinyo unaotengenezwa na zabibu zilizolimwa nje ya nchi kwa kiwango kinachozidi asilimia 25 kutoka Sh 2,130 kwa lita mpaka Sh 2,237. Vinywaji vikali, havikuachwa nyuma maana ushuru umepanda kutoka Sh 3,157 mpaka Sh 3,315.

Sigara 
Sigara zisizo na kichungi zinazotengenezwa kwa tumbaku ya hapa nchini kwa kiwango angalau asilimia 75 kutoka Sh 11,289 hadi Sh 11, 854 kwa kila sigara 1,000. 
Kwa upande wa sigara zenye kichungi zinazotengenezwa kwa tumbaku ya nchini kwa angalau asilimia 75, ushuru juu kutoka Sh 26,689 hadi Sh 28, 024 kwa kila sigara 1,000. 
Sigara zenye sifa tofauti na hizo, ambazo hazina vigezo hivyo vya tumbaku ya ndani, ushuru wake umepanda kutoka Sh 48,285 hadi Sh 50,700 kwa kila sigara 1,000.

Katika tumbaku ambayo iko tayari kutengenezwa kuwa sigara, ushuru wake umeongezeka kutoka Sh 24,388 hadi Sh 25,608 kwa kilo huku ushuru wa sigara aina ya Sigar ukibaki kuwa asilimia 30. 
Vilainishi, gesi asilia, simu juu 
Katika mafuta ya kulainisha mitambo, ushuru umepanda kutoka Sh 665.50 kwa lita hadi Sh 699 kwa lita, huku ushuru wa grisi za kulainisha mitambo, ukipanda kutoka senti 75 kwa kilo, hadi senti 79 kwa kilo.

Gesi asilia pia ushuru umepanda kutoka senti 43 kwa futi za ujazo mpaka senti 45 kwa futi za ujazo. 
Kuhusu viwango vya ushuru wa kuhamisha fedha kwa kutumia simu, serikali imependekeza kutoza ushuru wa asilimia 10, kwenye ada zinazotozwa na watoa huduma wa simu, katika kutuma na kupokea fedha, badala ya ushuru huo kutozwa tu katika kutoa fedha.

Kwa mujibu wa Dk Mpango, kwa utaratibu wa sasa, baadhi ya kampuni zinazotoa huduma zimetumia mwanya wa kuhamisha sehemu kubwa ya ada hizo kwenye kupokea fedha na hivyo kuwa nje ya wigo wa kodi. 
Ulaji wa wabunge, hisa
Kwa upande wa kiinua mgongo cha wabunge wakati wa kustaafu, sasa kitatozwa kodi kila mwisho wa muhula wa miaka mitano ili kujenga misingi ya usawa na haki katika utozaji wa kodi kwa kila mtu anayestahili kulipa.

Aidha, mapato yote yatokanayo na hisa katika kampuni mbalimbali sasa yatatozwa kodi, baada ya kufutwa kwa msamaha kwa waliokuwa wakimiliki hisa chini ya asilimia 25.
Kodi ya mishahara 
Katika kodi inayokatwa katika mishahara (P.A.Y.E), imepunguzwa kutoka asilimia 11 mpaka tisa kwa wafanyakazi wanaopata mshahara wa kuanzia Sh 170,000 lakini hauzidi 360,000. Kwa wanaopata zaidi ya 360,000 lakini haizidi 540,000, watakatwa Sh 17,100 pamoja na asilimia 20 ya kiasi kinachozidi Sh 360,000.

Kabla ya hapo walikuwa wakikatwa Sh 20,900 na asilimia 20 ya kiasi kinachozidi Sh 360,000. 
Wanaopata zaidi ya Sh 540,000 lakini haizidi Sh 720,000, watakatwa Sh 53,100 pamoja na asilimia 25 ya kiasi kinachozidi 540,000. 
Kabla ya hapo, walikuwa wakikatwa Sh 56,900 na hiyo asilimia 25 ya kiasi kilichozidi 540,000. Kwa wanaopata zaidi ya Sh 720,000 wao watakatwa Sh 98,100 pamoja na asilimia 30 ya kiasi kinachozidi Sh 720,000.

Kabla ya hapo, walikuwa wakikatwa Sh 101,900 pamoja na asilimia 30 ya kiasi kilichozidi Sh 720,000. 
Kodi za nyumba 
Serikali pia imependekeza malipo ya kupanga nyumba, nayo yatozwe kodi ambayo haikuweka kiwango, ila imependekeza Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato, apewe mamlaka ya kukadiria kiwango cha chini na cha juu cha mapato yapatikanayo na pango ili yatozwe kodi.

Kodi za nyumba, usajili magari, pikipiki 
Mbali na mapato ya kodi za nyumba, Serikali imependekeza kupandisha ushuru wa kusajili magari na pikipiki kutoka Sh 150,000 hadi Sh 250,000 kwa kila gari na kutoka Sh 45,000 hadi Sh 95,000 kwa kila pikipiki. 
Kwa watumiaji wa namba binafsi za magari, ada sasa itapanda kutoka Sh milioni 5 kila baada ya miaka mitatu mpaka Sh milioni 10.

Kodi ya majengo 
Aidha, kodi za majengo sasa hazitakusanywa na halmashauri, badala yake TRA ndiyo inayopewa mamlaka hayo ya kukadiria, kukusanya, kuhifadhi na kuiwakilisha katika halmashauri husika. 
Mbali na TRA kupewa mamlaka ya kukusanya kodi ya majengo, serikali pia imependekeza kupunguza misamaha ya kodi za majengo ili majengo mengi zaidi yaingizwe katika orodha ya kulipa kodi.

Ulindaji wa Viwanda 
Saruji aina ya (HS Code 2523.29.00) zinazotoka nje ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ushuru wake wa forodha umepandishwa kutoka asilimia 25 mpaka asilimia 35 ili kulinda saruji inayozalishwa nchini dhidi ya ushindani wa bei ya saruji kutoka nje ya nchi.

Kwa bidhaa za chuma ikiwemo mabati kutoka nje ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, nazo ushuru umetoka asilimia 0 mpaka 10, ili kulinda uzalishaji wa bidhaa hizo hapa nchini, huku bidhaa za nondo kutoka nje nazo zikipandishwa kodi kutoka asilimia 10 mpaka 25, kwa nia ya kulinda viwanda vya ndani.

Nyavu za kuvua samaki kutoka nje ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, ushuru wake umepanda kutoka asilimia 10 hadi asilimia 25 huku vichujia vya vilainishi na petroli kutoka nje ya nchi vikiongezwa ushuru kufikia asilimia 25 kutoka asilimia 10, ili kulinda bidhaa za ndani.

Sukari, ngano, mitumba, mafuta ya kula 
Katika sukari, serikali imekusudia kupunguza msamaha wa kodi na hivyo waagizaji wa bidhaa za sukari kutoka nje watalazimika kuanza kulipa ushuru wa asilimia 15 kutoka asilimia 10, huku ikitarajiwa kuongezeka zaidi na kuwa asilimia 20 mwaka 2017/18 na asilimia 25 mwaka 2018.19, ili kulinda viwanda vya ndani.

Kwa upande wa ngano kutoka nje, ushuru umepunguzwa kutoka asilimia 35 mpaka 10, kwa kuwa nchi za Afrika Mashariki hazina uwezo wa kuzalisha kulingana na mahitaji. 
Kwa upande wa nguo na viatu vya mitumba Serikali imepandisha ushuru kutoka dola za Marekani 0.2 mpaka dola za Marekani 0.4 kwa kilo, kwa nia ya kudhibiti nguo hizo lakini pia imetangaza kujiandaa kuzuia uingizaji wake.

Kwa upande wa mafuta ya kula kutoka nje nayo ushuru umepanda kutoka asilimia 0 mpaka 10 kwa mafuta ghafi ya kula, ili kuimarisha kilimo cha mbegu za mafuta na viwanda vya ndani. 
Tozo za pamba, kahawa, korosho 
Miongoni mwa tozo zilizofutwa kuondoa kero kwa wananchi ni mchango kwa kila kiwanda cha kuchambua pamba wa Sh 450,000 na ada ya vikao vya halmashauri wakati wa kujadili wafanyabiashara wa pamba ya Sh 250,000.

Kwa upande wa kahawa, Serikali imefuta ada ya leseni ya kusindika kahawa ya dola za Marekani 250, huku ushuru wa kusafirisha korosho wa Sh 50 kwa kilo, ukifutwa. 
Tozo zingine zilizofutwa katika korosho ni ushuru wa chama kikuu cha ushirika Sh 20 kwa kilo, gharama za mtunza ghala Sh 10 kwa kilo, kikosi kazi cha kufuatilia masuala mbalimbali Sh 10 na makato ya unyaufu.

Pia Serikali imepanga kuendelea kufuta tozo nyingine zinazokatwa na halmashauri, wakala na mashirika katika mazao ya wakulima, baada ya kufanya tathmini za kina.
Maduka kambi za jeshi 
Serikali imependekeza kufuta msamaha wa kodi uliokuwa ukitolewa katika maduka na migahawa maalumu kwa ajili ya askari wa majeshi, kutokana na msamaha huo kutumiwa vibaya na kupoteza mapato ya serikali na badala yake, askari watapata posho mpya juu ya posho ambazo wamekuwa wakipewa.

Jumanne, 7 Juni 2016

MCHAKATO WA UCHAGUZI WA YANGA WABARIKIWA NA JAMAL MALINZI

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), leo Juni 7, 2016 limefanya kikao cha pamoja na uongozi wa Klabu ya Young Africans.

Kikao hicho kilifanyika ofisi ya TFF iliyoko Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Ilala jijini Dar es Salaam na kuongozwa na Rais wa TFF Jamal Malinzi kilihudhuriwa na Katibu Mkuu wa TFF, Mwesigwa Selestine; Kaimu Mkurugenzi wa Sheria na Uanachama, Elliud Mvella; Makamu Mwenyekiti wa Young Africans, Clement Sanga na Katibu Mkuu wa Young Africans, Baraka Deusdedit.

Baada ya mazungumzo, Rais wa TFF, Malinzi ametoa maelekezo yafuatayo:-
1.   Mchakato wa Uchaguzi wa Young Africans uendelee.
2.   Mchakato huo usimamiwe na Kamati ya Uchaguzi ya Young Africans chini ya uangalizi wa Kamati ya Uchaguzi ya TFF.
3.    Wale wote waliochukuliwa fomu za uchaguzi wa Young Africans katika ofisi za TFF washirikishwe kwenye mchakato huo.
Mwisho, Rais wa TFF Jamal Malinzi amewatakia kila la kheri wanachama na  wapenzi wa Young Africans na kuwa na umoja na mshikamano kuelekea uchaguzi huo muhimu wa kwa mustakabali wa klabu.

Jumapili, 5 Juni 2016

UMOJA WA MATAIFA WAPONGEZA UTENDAJI WA RAIS MAGUFULI


SHIRIKA la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), limeeleza kuridhishwa kwake na utendaji wa Rais John Magufuli katika mapambano ya rushwa, kuongeza uwajibikaji na ukusanyaji wa mapato.

Mwakilishi Mkazi wa UNDP nchini, Alvaro Rodriguez, alisema hayo jana katika semina ya wabunge kuhusu Malengo 17 ya Maendeleo Endelevu ya Dunia.

Alisema Serikali ya Awamu ya Tano, imekuwa ikipambana na rushwa na kusimamia kwa karibu ukusanyaji mapato, hali aliyosema itasaidia maendeleo kwa kuwa hakuna nchi iliyoendelea bila kuchapakazi.

Rodriguez alisema mbali na kuona maendeleo katika baadhi ya mikoa na mitaa, ameona jitihada hizo za Serikali na amefurahishwa na kuridhika nazo.

Mwakilishi huyo pia alisema Serikali ya Tanzania na Ofisi ya Umoja wa Mataifa (UN), zimekuwa zikifanya kazi pamoja katika harakati za usambazaji wa malengo ya dunia kwa Watanzania.

Alisisitiza umuhimu wa malengo hayo kueleweka kwa wabunge, ili katika jukumu lao la kuisimamia Serikali, wawe mabalozi wa utekelezaji wa malengo hayo katika ufuatiliaji kwenye ngazi zote za utawala.

Awali akifungua semina hiyo, Naibu Spika wa Bunge, Dk Tulia Ackson aliwataka wabunge kuoanisha malengo hayo na malengo ya Dira ya Taifa ya 2025 pamoja na malengo ya Mpango wa Taifa wa Miaka Mitano wa 2016/2017 mpaka 2020/2021 ambao ulishafikishwa bungeni.

Dk Tulia aliwataka wabunge kila mmoja kuyaelewa vizuri malengo hayo ili kila mmoja ashikilie mahali atakapofuatilia Serikalini wakati wa utekelezaji wake.

Miongoni mwa malengo hayo ni pamoja na kutokomeza umasikini wa kila aina, kufuta njaa kwa kuhakikisha kuna kuwa na uhakika wa chakula bora kwakuboresha kilimo endelevu, kuhakikisha watu wote wanakuwa na afya bora nakupata huduma za afya na kupunguza utofauti wa kipato.

Akitoa mada katika semina hiyo, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Paul Kessy, alisema Tanzania imeshiriki kwa kiasi kikubwa katika maandalizi ya malengo hayo na hivyo mchango wake kuwa sehemu ya maudhui ya malengo hayo endelevu kwa maslahi mapana ya taifa na watu wake.

Kwa mujibu wa Kessy, sehemu ya mchango wa Tanzania katika kuunda malengo hayo, ilikuwa ni kutaka malengo hayo yahakikishe kuwa baadhi ya masuala ambayo hayakukamilika katika utekelezaji wa Malengo ya Milenia yanazingatiwa katika malengo endelevu.

Baadhi ya mambo hayo ni pamoja na kupunguza umasikini, upatikanaji wa ajira na kukuza uwezo wa nchi masikini hasa katika maendeleo ya teknolojia.

JAMES MWAMPONDELE ASHINDA UKATIBU UCHUMI NA FEDHA MKOA WA MBEYA


Ccm mkoa wa Mbeya na Songwe umefanya uchaguzi iliyokuwa wazi ya Ukatibu wa uchumi na fedha baada ya aliekuwa mwenye nafasi hiyo kufaliki toka mwaka jana.Katibu mpya wa uchumi na fedha amepatikana jana. James Mwampondele kushinda kwa kura 36 akifuatiwa na Mwakajumilo aliepata kura 25 na Charles Mwakipesile aliepata kura 4 hata hivyo baada ya kutangazwa mshindi Mwampondele alisema cha kwanza ni kuanza kutoa semina kwa wajumbe wote ,na kuanza kufuatilia miradi ya chama yote.

Ijumaa, 3 Juni 2016

WAPINZANI WAANIKA SABABU SITA ZA KUMKATAA NAIBU SPIKA


Wabunge wa upinzani wameendelea kususia kwa siku ya tatu mfululizo vikao vya Bunge vinavyoendeshwa na Naibu Spika, Dk Tulia Ackson tangu walipotangaza hatua hiyo Jumatatu wiki hii kwa kutokuwa na imani naye.

Tangu Jumanne wiki hii wabunge hao wamekuwa wakisusa vikao vinavyoongozwa na kiongozi huyo kwa madai kuwa anaminya demokrasia.

Siku hiyo wabunge hao waliingia bungeni kama kawaida na Dk Tulia alipomaliza tu kusoma dua ya kuliombea Bunge, walitoka hadi kipindi hicho kilipomalizika na naibu spika kumwachia mwenyekiti wa Bunge, Andrew Chenge kuongoza, ndipo wote waliporudi ukumbini na kuendelea na shu ghuli zao kama kawaida. 

Juzi, wabunge hao wote kama kawaida waliingia bungeni asubuhi na alipoingia Dk Tulia kuongoza kikao hicho, walisimama na kusikiliza dua ya kuliombea Bunge, kisha walitoka na kuwaacha wabunge wa CCM wakiendelea na Bunge.

Siku nzima ya juzi ambayo Dk Tulia aliendesha kikao cha asubuhi na jioni, wabunge hao hawakuhudhuria na ilipofika wakati wa kusoma hotuba ya msemaji wa kambi ya upinzani kwa Wizara ya Fedha na Mipango, David Silinde aliingia ukumbini akitokea nje na kuomba hotuba yake iingie kwenye kumbukumbu rasmi za Bunge kama ilivyo. Kisha akasema: “Sitaisoma hapa kwa kuwa haturidhishwi na mwenendo wa Naibu Spika wa kutuendesha kama watoto.”

Wabunge hao wa upinzani walitoa sababu sita kwanini wanataka Dk Tulia aondolewe madarakani kwa Azimio la Bunge.

Akizungumza na waandishi wa habari jana kwa niaba ya wabunge hao, Mbunge wa Simanjiro, James Millya alizitaja sababu hizo kuwa ni kwanza Dk Tulia ameweka maslahi ya chama chake cha siasa mbele kuliko maslahi ya Bunge, kinyume na Kanuni ya 8(b) ya Bunge.

“Pili, Mei 6 alitumia vibaya madaraka ya kiti cha Spika kwa kutoa uamuzi wa mwongozo ambao ulikuwa unakiuka Ibara ya 12(2) ya Katiba. Muongozo huo uliokuwa unapinga udhalilishaji wa wabunge wanawake,” alisema.

Ya tatu ni kitendo cha Dk Tulia kuvunja Kanuni ya 64(1) (f) na (g) zinazokataza mbunge kutumia lugha ya matusi kwa mbunge mwingine ambapo alinukuliwa akisema “Mheshimiwa Bwege, usionyeshe ubwege wako humu ndani.” 

Alisema ya nne ni Mei 30 kiongozi huyo aliamua kwa makusudi kuvunja Ibara ya 63(2) ya Katiba na kutumia vibaya Kanuni ya 69(2) na 47(4) ya Kanuni za Bunge kumzuia Joshua Nassari kwa upande mmoja na Bunge zima kwa upande wa pili kutimiza majukumu yake ya kikatiba ya kusimamia na kuishauri Serikali.

“Sababu ya tano ni kuwa Mei 26, mwaka huu Dk Ackson akiongoza kikao cha Bunge bila ridhaa ya upinzani alishiriki kufuta sehemu ya hotuba ya msemaji wa upinzani kwa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kinyume cha kanuni ya 99(9) ya Bunge bila kushirikisha kamati yoyote ya Bunge,” alisema.

Sababu ya sita, Millya alisema kuwa ni kitendo cha Dk Ackson kukataa taarifa ya maoni tofauti, iliyowasilishwa na wabunge wanne wa upinzani.