Jumamosi, 18 Aprili 2015

YANGA WALAZIMISHWA MOJAMOJA



Etoil Du Saheil ya Tunisia wamefanikiwa kupata sare ya goli 1-1 mbele ya vinara wa ligi kuu ya vodacom Yanga, katika mchezo wa kombe la shirikisho barani Afrika.

Katika mchezo huo wa kwanza katika hatua ya pili ya michuano hiyo uliofanyika katika uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam hii leo, Yanga waliuwanza mchezo kwa kasi na katika dakika ya pili walifanikiwa kupata penati.

Penati hiyo ilitokana na kufanyiwa madhambi kwa Saimon Msuva katika eneo la hatari, na yanga kuandika goli la kuongoza kwa mkwaju huo wa penati uliopigwa na nahodha Nadir Haroub 'Canavaro' katika dakika hiyo ya pili ya mchezo.

Kuingia kwa goli hilo kulipelekea wa Tunisia Etoil Du Saheil kulisakama lango la yanga kwa dakika zote 43 za kipindi cha kwanza huku yanga wakipeleka shambulio moja moja katika dakika zote za kpindi cha kwanza kilichosalia.

Katika dakika 2 za mwisho za kipindi cha kwanza kama yanga wangekuwa makini wangeweza kupata goli la pili, lakini hadi dakika 45 za kwanza zinamalizika Yanga 1-0 Etoil Du Saheil.

Kipindi cha pili kilianza kwa yanga kumpumzisha nahodha Nadir Haroub Cannavaro na nafasi yake kuchukuliwa kwa Said Juma Makapu, mabadiliko yaliyoleta utulivu katika eneo la kati kwa upande wa yanga.

Katika dakika ya 47 Etoil Du Saheil walisawazisha goli hilo na kupelekea kuanza kucheza kama hawataki, huku wakitumia muda mwingi kulinda matokeo hayo, ambapo kulipelekea mchezo kuonekana kuwa sawa na yanga kufanikiwa kufika langoni mwa Etoil Du Saheil mara kadhaa.

Hadi dakika 90 zinakamilika Yanga goli 1 na Etoil Du Saheil goli 1, na hivyo kuiweka yanga katika mazingira magumu katika mchezo wa marejeano utakao fanyika nchini Tunisia wiki mbili zijazo, ambapo Yanga watahitaji ushindi ama sare ya kuanzia goli 2 ili wapite.