Jumapili, 3 Mei 2015

SIMBA MAMBO SAFI YAIADABISHA AZAM SASA YASUBIRI MBELEKO ZA YANGA


Simba SC imeendelea kuitafuta kwa nguvu nafasi ya pili ya ligi kuu nchini Tanzania baada ya kuwashikisha adabu wana lambalamba Azam FC kwa kuwabamiza bao 2-1 katika mchezo mkali wa ligi kuu ya Vodacom Tanzania bara.

Simba ambayo sasa imefikisha pointi 44 pointi moja nyuma ya Azam FC wanaokamata nafasi ya pili wakiwa na pointi 45 huku Simba wakiombea Azam wafungwe na Yanga Jumatano ili nafasi ya kuwania mshindi wa pili ibaki katika siku ya mwisho.

Magoli ya Simba leo yalifungwa na Ibrahim Ajib na Ramadhani Singano maarufu kama Messi wakati Azam wakipata bao lao la kufutia machozi kupitia kwa Mudahir Yahya.

Azam walimpoteza nahodha wao Salum Abubakar "Sure boy" baada ya kupata kadi mbili za njano zilizopelekea kupata kadi nyekundu dakika ya 38.
Azam itacheza na Yanga Jumatano wiki hii na kama ikishinda basi itakamata nafasi ya pili.