Jumanne, 2 Juni 2015

Prof. Mwandosya ametangaza nia yake ya kuomba kuteuliwa na chama cha mapinduzi kugombea nafasi ya urais.

Waziri wa nchi, ofisi ya rais kazi maalum, Prof. Mark Mwandosya ametangaza nia yake ya kuomba kuteuliwa na chama cha mapinduzi kugombea nafasi ya rais kwenye uchaguzi mkuu ujao, huku akisema kuwa endapo atapata ridhaa hiyo, kipaumbele chake kitakuwa ni kujenga uchumi imara wa taifa na watanzania kwa ujumla.
Waziri wa nchi, ofisi ya rais, kazi maalum, Prof Mark James Mwandosya,jana amesimama mbele ya umati mkubwa wa wakazi wa jiji la Mbeya na kutangaza rasmi nia yake ya kutaka kukiomba chama chake, chama cha mapinduzi kumteua kuwa mgombea wake wa nafasi ya urais kwenye uchaguzi mkuu ujao.
Prof. Mwandosya ambaye pia ni mbunge wa jimbo la Rungwe mashariki, kupitia hadhira hiyo akatangaza kuwa endapo watanzania watampa ridhaa ya kuwaongoza kama rais, kipaumbele chake kitakuwa ni kujenga uchumi imara wa taifa na watanzania kwa ujumla.
Kabla ya Prof. Mwandosya kutangaza nia yake, baadhi ya viongozi wa dini, viongozi wa mila na wanasiasa wakapewa nafasi ya kuzungumza, ambapo wengi wao wamedai kuwa Prof. Mwandosya amelitumikia taifa kwa muda mrefu bila kuwa na kashfa ya aina yoyote, hivyo anastahili kuliongoza taifa la Tanzania.
Prof. Mwandosya ametangaza kwenda kuchukua fomu Dodoma siku ya jumatano wiki hii ambapo zaidi ya shilingi milioni 10 zilichangwa na wananchi kwa ajili ya kumuwezesha kuchukua fomu hiyo.